Saturday, 27 July 2013

Bado Watanzania wengi wanatumia futi

Beniel Seka

Futi ni moja ya vipomo ambayo vimeendelea kuwepo katika mfumo wa upimaji tangu tupate uhuru hadi sasa. Kipimo hiki kilichokuwa katika mfumo wa Kiingereza uliojulikana kama “imperial units” bado kinatumiwa kwa kiasi kikubwa na mafundi uashi, useremala na mafundi bomba.

Baada ya uhuru Tanzania iliamua kutumia mfumo wa metriki ambao kigezo kikuucha urefu  ni meta(m). Vigezo vingine vinavyoambatana na meta ni milimeta (mm), sentimeta(cm) na desimeta(dm) ambavyo ni vidogo kuliko meta. Katika mpangilio huo milimeta ndio kiwango kidogo kuliko vyote. Vingine  ni dekameta(dm), hektometa(hm) na kilometa(km). Katika mpangilio wa ukubwa kilometa ndio kiwango  kikubwa kuliko vyote.

Mfumo huu wa metriki hutumiwa na nchi nyingi duniani. Kinachoufanya ukubalike na nchi hizo ni urahisi ulioko katika kuhama kigezo kimoja kwenda kingine. Kutoka kigezo kimoja kikubwa kwenda kingine cha chini kinachofuata, unazidisha kwa kumi. Kutoka kigezo kimoja kidogo kwenda kingine cha juu kinachofuata, unagawanya kwa kumi. Kwa mfano, kubadili kilometa kuwa hektometa,  unazidisha kwa kumi, yaani kilometa moja ni hektometa 10. Kubadili milimeta kuwa sentimeta unagawanya kwa kumi kwa kuwa  milimeta 10 ni sentimeta 1.

Shule za Tanzania hufundisha mfumo huo wa metriki. Mifumo mingine hutajwa tu kwa ajili ya kulinganisha, lakini si kwa nia ya matumizi. Utafiti umeonesha kuwa wanafunzi hawana tatizo na mfumo wa metriki. Walimu wengine wamekwishawapatia hata njia za kukumbuka mpangilio ili kurahisisha kubadili kigezo kimoja hadi kingine. Kwa mfano, sentensi: ‘Mimi sili dagaa maana daima hupata kichefuchefu (mm,sm,dm,m,dam,hm,km)’. Pamoja na sentensi hiyo kuwa kejeli, lakini husaidia kukumbuka uhusiano wa vigezo hivyo.

Tatizo ni nini hasa? Tatizo lipo kwa jamii. Bado watu wengi katika jamii ya Tanzania hawatumii mfumo huu. Kama ulivyokwishaona hapo mwanzo mwa makala hii, watu wengi wanatambua na kutumia futi badala ya meta. Utasikia fundi seremala akizungumzia kitanda cha futi sita kwa sita au bati la futi 10. Vigezo vingine katika mfumo huu ni yadi, cheini, maili na inchi. Utasikia kwa mfano, fundi akisema “nipe misumari ya inchi nne” au “bomba la nusu inchi”.

Matumizi hayo humchanganya  mwanafunzi ambaye hakufundishwa vipimo hivyo. Mwanafunzi anaona kuwa mambo ya shuleni hayana matumizi ndani ya jamii. Anafikiri anayojifunza shuleni ni kwa ajili ya taaluma tu. Mazingira ya namna hiyo humfanya mwanafunzi asifurahie masomo kwa kuwa yanaishia darasani tu.Baadhiya mafundi waliwahi kuomba mtindo wa vipimo vya Waingereza vifundishwe sanjari na vile vya metriki.

Tatizo jingine analokumbana nalo mwanafunzi ni kutokijua kipimo. Hajui yadi ina urefu wa kufananishwa na kitu gani. Anajua meta inakaribia urefu toka sakafuni  hadi kiunoni anapokuwa amesimama. Hajui inchi ina urefu unaofananishwa na nini. Anajua sentimeta inalingana kwa urefu na ukucha wa kidole gumba. Hajui futi, lakini walau hii anaiona kwenye rula zilizotengenezwa kwa urefu huo na zinatumika darasani. Hajui maili lakini anajua kilometa moja ni umbali kutoka wapi hadi wapi. Anajua kutoka nyumbani kwenda hadi shuleni ni umbali wa kilometa ngapi. Yote hayo amejifunza shuleni.

Waingereza walipotengeneza mfumo wao wa upimaji walihusisha mambo yao. Kwa mfano, wana kizio kinachoitwa dazeni chenye dhana ya 12. Ndio sababu wakaweka kigezo cha inchi na kusema inchi 12 ni sawa na futi moja. Neno ‘futi’ ni neno lililotoholewa kutoka neno la kiingereza ‘foot’ ambalo lina maana ya unyayo, lakini tusiingie huko. Ishirini ni kizio kingine walichokitumia Walikuwa na kigezo cha uzani walichokiita ‘hundredweght(cwt)’. Tani moja ilikuwa na cwt 20.

Waliteua yadi kuwa futi tatu. Kwa nini tatu ikatumika wanajua wao. Pengine inatokana na misahafu.  Katika mantiki hiyo ukikokotoa unapata yadi moja ni sawa sawa na inchi 36, yaani  12 x 3. Halafu wakaja na kigezo cha cheini; pengine kwa sababu maalum. Cheini ni yadi 22. Kisha waliteua maili kuwa na cheini 80 ambazo ni sawasawa na yadi 22 x 80 = yadi 1760. Pia kulikuwa na kigezo kilichoitwa ‘furlong’ ambapo furlon moja ilikamilisha urefu wa futi 660 au cheini 10.

Wakati wanatutawala walitufanya tuone kwamba vipimo vya mfumo wao vilikuwa bora zaidi. Walitukaririsha vipimo hivyo vikaendelea kudumu ndani ya fikra za wengi waliosoma enzi hizo. Matumizi yalifanikiwa kwa kiasi kikubwa kwa kutumia mfumo huo kwa sababu mfumo wa metriki haukupewa kipaumbele.

Waingereza hao na washirika wao kama Marekani, bado wanatumia mfumo huo. Walijua fika kwamba Watanganyika hatimaye wangekutana na huo mfumo wa metriki. Waliandaa katika majalada ya madaftari, orodha za kubadili vipimo vyao kwenda vipimo vya metriki. Kwa mfano:

Inchi 1 = sentimeta 2.54
Meta 1 = inchi 39.37
Maili 1 = kilometa 1.6
Yadi 1 = sentimeta 91.44
 
Ukokotoaji huo kwa ajili ya kubadili ulikuwa mgumu. Hii iliwafanya baadhi ya watu kuridhika na mfumo huo wa kiingereza na kutotilia maanani mfumo rahisi wa metriki. Hili ndilo tatizo kubwa tulilorithi kwa hao wakoloni. Kuna wakati baadhi ya mafundi waliomba mfumo huo urejeshwe maana wanafunzi waliomaliza darasa la saba walikuwa wanashindwa kumudu mafunzo ya fani kadhaa za ufundi yaliyokuwa yanatumia mfumo wa vipimo vya Waingereza. Ombi lao lilikataliwa na sasa wanalazimisha tu. Tuendelee namna hii mpaka lini?
Kwa wale waliozoea vipimo hivyo vya Waingereza wanaweza kuanza kulinganisha ifuatavyo: Futi 10= meta 3; futi 8=meta 2 na nusu; futi 5= meta 1 na nusu; inchi 4 = sm 10 na maili 5 ni sawa sawa na kilometa 8. Badala ya kutengeneza kitanda cha futi 6  ambavyo ni karibu meta 2, mafundi wangetengeneza vya meta 2, na kadhalika.

Viwanda vingi hapa nchini sasa vinatengeneza bidhaa kwa vipimo vya metriki. Hata Waingereza na washirika wao wameanza kutengeneza bidhaa zao kwa vigezo vya metriki kuwahi soko la kimataifa. Kwa nini wewe uendelee kung’ang’nia vipimo vyao? Nashauri uachane nao. Nenda na wakati.


END

No comments:

Post a Comment