Saturday, 27 July 2013

KADIRIO LA PAI LAFANYIKA KIMYAKIMYA

BENIEL SEKA

Tarehe 22 Julai ni siku ya kadirio la pai. Huenda siku hiyo imepita bila wengi wenu kugundua. Hii inawezekana imetokana na baadhi yenu kutojua kuwepo kwa siku hiyo au siku hiyo kutokuwa na shamrashamra za kuifanya ijulikane. Hata hivyo makala hii inakusudia kukufahamisha kuhusu siku hiyo ili wakati ujao uweze kuienzi au kuisherehekea.
     Wengi wenu bila shaka mtakumbuka kwamba tarehe 14 Machi ni siku ya pai. Hii inatokana na thamani ya pai kwa nafasi mbili za desimali ambayo ni 3.14. Tatu inatumika kuwakilisha mwezi wa 3 wa mwaka ambao ni Machi na 14 inawakilisha siku ya 14 ya mwezi huo. Siku hiyo ilipendekezwa na walimu wa hisabati kwa mara ya kwanza huko San Frasisco Marikani na kuungwa mkono na wanahisabati katika nchi kadhaa duniani. Tanzania ilianza kuisherehekea siku hiyo tangu 2004.
     Kuanzishwa kwa siku hiyo kuliamsha mjadala kwa nini 3.14 ipewe siku maalumu wakati kuna kadirio jingine la pai ambalo ni 22 juu ya saba. Hata wanafunzi shuleni huambiwa pai ni 22 juu ya 7 au 3.14. Namba hizo mbili hutumika wakati wa kukokotoa eneo la umbo duara, mzingo wa duara, eneo na ukubwa (ujazo) wa mche duara na kadhalika. Kwa mantiki hiyo, ilikubaliwa kuwe na siku nyingine kwa ajili ya pai ambayo ilipendekezwa iwe 22 Julai na iitwe SIKU YA KADIRIO LA PAI.
     Kwa wale ambao mmekuwa mnafuatilia sherehe za pai mtakumbuka kwamba Tanzania imekwisha sherehekea siku ya pai kwa mara tisa na. kiasi miaka inavyokwenda ndio msisimko wa pai unavyoongezeka na sherehe kuzidi kufana. Wale mlioshnudia sherehe ya mwaka huu mnakumbuka jinsi walimu, wanafunzi , wahadhiri wa vyuo vikuu, wakufunzi wa vyuo vya ualimu na wadau mbalimbali walivyofanya matembezi ya hiari kutoka shule ya sekondari ya Jangwani hadi viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam. Taasisi ya Elimu Tanzania iliratibu sherehe hii hadi 2006. Kuanzia mwaka 2007 sherehe hii imekuwa ikiendeshwa na Chama cha Hisabati Tanzania (CHAHITA).
      Tofauti na sherehe ya siku ya pai, CHAHITA hakiratibu sherehe ya siku ya kadirio la pai. Sherehe hiyo imeachwa kuwa huria. Shule na Taasisi zenye mapenzi na hisabati zinaweza kufanya sherehe hiyo kwa mikakati ambayo itasaidia kuhamasisha wanafunzi kupenda somo la Hisabati. Pengine kukosekana nguvu ya kitaifa ya CHAHITA ndiyo chanzo cha watu wengi kutoijua siku hiyo lakini hata juhudi za binafsi husaidia.
       Miaka michache iliyopita, mwalimu Eva Kwalazi Kipimo wa Shule ya Msingi Uhuru Wasichana,  aliwahi kufanya sherehe hiyo katika Shule ya Uhuru Wasichana wakati alipokuwa anafundisha hapo. Sasa ni mstaafu. Yeye aliita SIKU YA HISABATI na shule iliwaalika wazazi kuona matukio mbalimbali ya Hisabati pamoja na zana za kufundishia/kujifunzia somo hilo.
     Baadhi yenu mtajiuliza kwa nini tunasema kadirio la pai. Kwani thamani halisi ya pai ipi? Ili uielewe hiyo inakubidi ujue pai ni nini, Pai si 22 juu ya 7  au 3.14 kama ulivyozoea kuamini. Haayo ni makadirio tu na yanatosheleza kwa matumizi ya kawaida. Thamani kamili kwa tarakimu  bado  haijapatikana. Wataalam wanaendelea kuitafuta  japoluwa imeshatafutwa kwa mamjilioni ya nafasi za desimali. Wanachotafuta ni kujua ni lini tarakimu zitaanza kujirudia ili wachunguze mtindo wa mtiririko na hatimaye kuunda kanuni.
     Kimsingi tunajua kuwa pai ni mzingo wa duara (mduara) gawanya kwa kipenyo chake. Unapogawanya unapata hisa kwa decimal. Si rahisi kuipata kwa sehemu. Unaweza kujaribu mwenyewe kwa kupima vitu vyenye umbo la duara. Pima mzingo kwa kuzungushia uzi  na hatimaye upime urefu wa uzi huo kwenye rula au metakamba.
      Pima urefu wa  kipenyo (kumbuka mstari wa kipenyo hupita katikati) kisha gawanya mzingo kwa kipenyo. Kadiria jibu lako kwa nafasi mbili za desimali. Fanya hivi kwa vitu kama vinne kaisha tafuta wastani. Kama umefanya kwa makini utapata jibu linalokaribia 3.14. Hilo ndilo kadirio lako la pai kwa kuwa umelitafuta mwenyewe na una haki ya kujivunia, au sio?
     Hebu sasa tuchunguze kadirio la 22 juu ya 7. Kwa nafasi tano za desimali, ukigawanya unapata 3.14286 wakati thamani halisi kwa nafasi hizo za desimali ni 3.14159. Unaona jinsi namba hizo zinavyotofautiana katika nafasi ya tatu ya desimali? Kwa hiyo 22 juu ya 7 ni kadirio la pai. Nadhani tumekwenda pamoja mpaka hapo.
      Sasa tuangalie utafanya nini siku hiyo mwakani.  Kama ni mwalimu utawakusanya wanafunzi na kuwapa fursa ya kuimba nyimbo za Hisabati. Unaweza kuandaa maonesho , kongamano au mdahalo  wenye uhusiano nna hisabati. Ikiwa wewe ni mkuu wa shule au chuo unaweza kualika mtaalamu wa Hisabati karibbu na wewe kuwahamasisha wanafunzi kupenda Hisabati. Ukiwa ni mdau wa kawaida changia mawazo yako kwa njia ya redio, televisheni na magazeti . Tutafurahia mchango wako.
Ni muhimukuzingatia hili maana wanafunzi wanahitaji kuhamasishwa  . Sote tumeshuhudia jinsi wanafunzi wanavyofeli katika somo la Hisabati kwenye mitihani ya Kitaifa. Fursa kama hii itumikekuinuan kiwango cha ufanisi kwa somo hilo.
    Mwaka huu magazeti mbalimbali yaliandka makala kuhusu siku ya Pai ioiyofanyika Mnazi Mmoja, Pia TBC1 plimwalika mtaalam wa pai kwenye kipindi cha Jambo asubuhj ya siku hiyo. Televisheni ya Channel Ten nayo ilirusha habari za kadirio hilo wakati wa mchana siku hiyo. Magazeti nayo yalilijizatiti kwa kuchapisha makala ya sikuya pai Tanzania.
 Mwalimu Albinus Balomi wa shule ya Sekondari Kijitonyama amekuwa miongoni  mwa watu wa kwanza kutoa mrejesho. Yeye alibahatika kuona hicho kipindi cha TBC1 wakati alipokuwa anajiandaa kwenda shuleni. “Nilifurahia sana maelezo yaliyotolewa  na mtaalamu. Alinifundisha mengi kuhusu pai kwa muda mfupi. Mimi ni mwalimu wa Historia na Jografia. Nilijiambia kwamba Hisabati inafundishika kutokana na jinsi mtaalamu huyo alivyowasilisha mada yake japo kwa muda mfupi tu. Wangemwongezea muda,” alidai mwalimu  Albinus.
 “Nilipokuwa njiani,” aliendelea kueleza, “nilinunua  magazeti. Nilikuta makala nzuri za Siku ya Kadirio la pai. Niliitumia kuwaelezea walimu wa Hisabati ambao kusema kweli hawakuwa wanaijua siku hiyo. Walihamasika sana”.
Kuna baadhi ya shule zimeonyesha kuijua hiyo siku ya kadirio la pai. Kwa mfano Shule ya Sekondari ya  Bright Angles iliyoko Mkuranga mkoa wa Pwani, iliahirisha sherehe ya siku hiyo hadi Jumamosi tarehe 27 Julai, ili iwashirikishe wazazi na wadau wengine. Shule imonyesha jitihada za kuhamasisha wanafunzi kupenda somo la Hisabati. Shule
imeamua kuwazawadia wanafuzi wote waliopata A katika mtihani wa  wa Taifa wa mwaka huu kwenye somo la Hisabati. Pia imemwalika mtaalamu mmoja wa Hisabati kuwahamasisha wanafunzi.
Kumbuka kuwa pai ina matumizi mengi katika maisha yetu. Hata kama hukuwahi kulipenda somo unaweza kutenga muda kidogo kuifurahia siku.

end

No comments:

Post a Comment