Saturday, 27 July 2013

Mtihani huu wa nini?

Beniel Seka
Mtihani wa kumaliza elimu ya msingi umekuwa na matatizo mengi. Hivi karibuni viongozi kadhaa wametoa malalamiko mengi kuhusu matokeo ya mitihani hiyo inayoendeshwa na Baraza la Mitihani la Taifa. Tatizo kubwa lililosababisha viongozi hao kuizungumzia mitihani hiyo ni jinsi matokeo yake yanavyotumika kuwezesha wanafunzi wasiojua kusoma au kuandikwa kujiunga na elimu ya sekondari.
Mitihani hiyo imelalamikiwa pia na wadau mbalimbali wa elimu ambao wanaona kwamba nchi yetu inaweza kupata wahitimu wasio na viwango vya kuridhisha ikiwa hali hii itaendelea . Wanahoji inakuwaje mwanafunzi asome kwa miaka saba bila kujua kuandika wala kusoma. Kinachowasikitisha zaidi ni kwamba mitihani hiyo inawathibitisha kuwa wamefaulu na wanastahili kuendelea na masomo ya sekondari.
Tatizo hili limejitokeza zaidi mwaka juzi  (2011), Baraza la Mitihani la Taifa lilipoanza kutahini somo la Hisabati kwa kutumia mtindo wa maswali ya kuchagua jibu sahihi. Tayari Chama cha Hisabati Tanzania (MAT/CHAHITA) kimeshatoa msimamo wake kupinga muundo huo wa mtihani katika somo la Hisabati. Aidha baadhi ya walimu na  wataalamu wengine wameshapendekeza kusitishwa kwa muudo huo wa kutahini Hisabati.
“Somo la Hisabati humhitaji mwanafunzi kuonesha njia aliyotumia kupata jibu,” alisema mwalimu mmoja mzoefu. Kisha aliedelea kueleza, “ Kuandika jibu peke yake hakusaidii kujua fikra alizo nazo mwanafunzi au uwezo wake wa kupangilia ufumbuzi wa tatizo, jambo ambalo ni muhimu sana katika kuelewa somo la Hisabati.”
Ni dhahiri kwamba mtihani huo wa kumaliza shule za msingi kwa sasa unashindwa kufanya kazi iliyokusudiwa. Kama watahiniwa wasio na uwezo, wakiwepo wasiojua kusoma wala kuandika, wanaweza kufaulu, basi ile nia ya kuutumia kuchagua wanafunzi bora imefifia. Tunajiuliza: kwani lazima mtihani huo uwepo? Hakuna namna nyingine ya kuwapata wanafunzi bora wanaostahili kuingia sekondari?
Kuna wakati mtihani huo ulikuwa muhimu maana ulikuwa mtihani pekee hapa nchini kwa ajili ya kuchagua wanafunzi  kuingia kidato cha kwanza katika shule za sekondari.  Wakati huo  hakukuwa na shule za sekondari za binafsi ukiacha zile za seminari ambazo zilikuwa na utaratibu wao wa kuchagua wanafunzi wa kujiunga na shule hizo. Baadaye ziliruhusiwa shule chache za binafsi. Hizi zilichagua wanafunzi wake baada ya zoezi la kuchagua wanafunzi wa sekondari za serikali kumalizika.
Kuanzishwa kwa shule nyingi za binafsi kulianza kufanya zoezi la kuchagua wanafunzi bora liingie dosari. Shule hizo za binafsi ziliingia katika ushindani wa kuwapata hao wanafunzi bora. Baadhi ya shule zilianza utaratibu wa kuwapa wanafunzi waliomaliza darasa la saba mtihani kabla ya matokeo ya mtihani wa taifa kujulikana. Kuna shule ambazo tayari zina umaarufu kiasi kwamba wanafunzi wakichaguliwa kuingia shule hizo hukataa  kuitikia ule wa shule za serikali. Hapo shule za sekondari kwa kiasi kikubwa huwakosa wale walioamua hivyo na husababisha uchaguzi wa pili kwa ajili ya kujaza nafasi zao. Huenda ndio sababu baadhi ya shule binafsi hufanya vizuri zaidi ya zile za serikali.
Hatushangai siku hizi kusikia kwamba baadhi ya shule za binafsi zinaongoza kwa kufaulisha wanafunzi katika mtihani wa kumaliza elimu ya sekondari. Kwa hiyo hapa tunaona kwamba wenye shule hizo wametumia mtihani mbadala kupata wanafunzi hao. Wala hawakuhitaji kuiita mitihani yao jina la ‘kitaifa’ kupata wateja. Umaarufu wa shule hizo ndio unafanya wanafunzi kutoka sehemu zote nchini kutafuta nafasi katika shule hizo. Hapo ndipo wanafanya mtihani pamoja na usaili.
Kitu kinachofanya mtihani wetu wa taifa uwe mgumu kufanikisha malengo ni gharama kubwa za uendeshaji kuanzia kutunga, kusimamia, kusahihisha hadi kuchakata matokeo. Baraza la Mitihani linapolalamikiwa kuhusu mtihani wa kuchagua jibu sahihi hujitetea kuhusu gharama. Ni kweli usahihishaji unakuwa umerahisishwa sana kutokana na kuwepo na tekinolojia inayowezesha usahihishaji kwa njia ya kompyuta. Lakini kwani lazima kufanya mtihani wa kitaifa? Shule nyingi zinazochukuwa wanafunzi hao ni za kata!

Kuna kanda za kielimu. Kwani mitihani hiyo haiwezi kuendeshwa kikanda? Hili ni kwa ajili ya kupunguza tu tatizo, lakini tukitaka kuboresha zaidi tunaweza kuiendesha  kimkoa au hata ngazi ya wilaya. Hapa tuna maana ya utunzi na hata usahihishaji. Nadhani ule mtihani wa darasa la nne ulikuwa unatumia njia hii. Kama ulisitishwa kwa sababu za gharama za uendeshaji, hapa nakaa kimya. Nisingependa turudie kosa.
Baada ya matokeo ya mwaka jana (2012) kutangazwa, tumefahamishwa kuwa wale waliochaguliwa kuingia kidato cha kwanza itabidi wafanye mtihani mwingine kubaini wale wasiojua kusoma wala kuandika. Kwani hawakujulikana kabla ya kufanya mtihani huo wa taifa? Kuna viongozi wa nchi waliwahi kuhoji inawezekanaje mtoto amalize elimu ya msingi bila kujua kusoma na kuandika? Tungerekebisha utaratibu huo mapema badala ya kuingia gharama za mtihani mwingine.
Pendekezo la mwisho ni kuachana na mtihani huo wa kumaliza elimu ya msingi. Tunajua kwamba kuna mitihani ya mihula ambapo wanafunzi wanapangwa kwa nafasi zao darasani na mzazi au mlezi  kupewa matokeo kumjulisha maendeleo ya mtoto. Najua baadhi yetu tutasema mitihani hiyo sio sanifu au haina viwango vya kuridhisha. Kama walimu watakuwa waaminifu na kutoa haki sawa kwa wanafunzi wote, njia hii inaweza kutoa matokeo sahihi zaidi ya yale tunayoshuhudia wakati huu. Tunachotakiwa kufanya ni kuongeza mafunzo ya utungaji wa mitihani kwa walimu wetu.
Labda baadhi yenu mnajiuliza wanafunzi watakaojiunga na sekondari za vipaji watapatikanaje. Hao watakuwa wameshaanza kujitokeza katika majaribio (testi) na mitihani ya mihula. Katika ngazi itakayoonekana inafaa , wanafunzi hao wenye vipaji wanaweza kupewa mtihani maalum ulio na vigezo vya kumtambua mwanafunzi kiuwezo. Tusaidiane kuondokana na tatizo hili la mtihani wa kumaliza elimu ya msingi. Tunahitaji wanafunzi bora na siyo bora wanafunzi kwa mendelezo wa elimu bora kwa ngazi zote. 


END

No comments:

Post a Comment