Beniel Seka
Waziri wa
Fedha Mheshimiwa Dk William Mgimwa (Mb) katika hotuba yake ya bajeti aliyotoa
bungeni tarehe 14 Juni 2012 huko Dodoma hakutaja neno trilioni hata mara moja. Pengine alikuwa na sababu maalumu za
kutolitumia neno hilo. Baadhi ya waliokuwa wanamtazama kwenye televisheni na
waliokuwa wanamsikiliza kwenye redio walijiuliza kwa nini amelikwepa neno hilo.
Tumemshuhudia
akisema: “bilioni elfu kumi na tano” kwa maana ya 15000000000000 badala ya “
trilioni kumi na tano” au kumi na tano trilioni ili kuitofautisha na
10000000000005. Aliendelea na mtindo huo wa kutaja bilioni pale ambapo angeweza
kusema trilioni. Sio kwamba alifanya makosa ila kwa nini alikuwa na msimamo huo
wakati kuna neno moja lenye maana ya bilioni
elfu moja? Hata hivyo alilitumia wakati wa kuhitimisha hoja. Labda alishauriwa
kufanya hivyo.
Baadhi ya
watazamaji na waliokuwa wanamsikiliza walipata taabu kiasi pale ambapo elfu ilipotumika
mara mbili kwa namba moja. Kwa mfano, “ bilioni
elfu mbili milioni na tatu elfu tisini tisini milioni(2003090000000) inasumbua
kuisoma”. Hii inasomwa : “trilioni mbili
bilioni tatu na milioni tisini.” Wale
waliokuwa wakiangalia matangazo hayo kupitia Star Tv na ITV waliweza kusoma
maneno chini ya luninga zao yaliyokuwa yametaja namba husika kwa trilioni
badala ya bilioni elfu.
Wakati wa
kuwasilisha bajei ya mwaka huu wa 2013/2014, Mheshimiwa Waziri Mgimwa
alilikwepa tena neno hilo hadi sehemu ya mwisho wa hotuba yake. Ilionekana wazi
jinsi kuacha kulitumia kulivyomsumbua kusoma tarakimu hizo na ilimlazimu
kurudia ili kueleweka. Lakini alipokuwa anafanya muhtasari alitaja neno hilo na
hakusumbuka tena. Kwa mfano alisema,”Bajeti ya mwaka 2013/2014 ni zaidi ya
trilioni kumi na nane”.
Wabunge
waliojadili hoja ya wazirimwaka jana na waandishi wa habari walitumia neno hilo
bila wasiwasi wowote. Ni neno linaloshika kasi kubwa katika bajeti yetu baada
ya bajeti yetu kufikia namba ya kiwango hicho. Tulikuwa na bajeti za mamilioni,
zikafuata za mabilioni na sasa tuko na bajeti za matrilioni. Sina uhakika kama
Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA)
limeshatoa neno mbadala kwa trilioni. Kama sio, basi litoholewe liwe rasmi.
Pengine
tatizo ni namna tunavyoliandika. Linaonekana kama neno la kigeni mno. Labda
lingekuwa na matamshi ya Kiswahili na kuwa tirilioni.
Vilevile si vizuri kutunga neno jipya kabisa kwa sababu trilioni ina mzizi
(au kiambishi awali) “tri” ambapo maana yake ni “tatu”. Ina maana tunaanza na
milioni kama “moja”, inafuatiwa na bilioni (bi ikiwa na maana ya “mbili” na hatimaye
trilioni. Ukiwa na milioni unazidisha kwa elfu kupata bilioni na ukiwa na
bilioni unazidisha kwa elfu kupata trilioni.
Inawezekana
kuwa mheshimiwa waziri alilenga watu wa kawaida na kuwaachia wasomi kutumia
wenyewe neno trilioni. Ninanasema hivyo kwa kuwa kiwango cha elimu ya msingi
kwa mujibu wa muhtasari wa Hisabati Darasa la Saba wa mwaka 2005 uliotolewa na
Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi ni bilioni. Hata hivyo kiwango hicho
kimewekwa kwa ajili ya ukokotoaji tu. Viwango vingine vinaweza kutumika kwa
kutumia stadi hizo hizo.
Ni vyema
kukumbuka namba za viwango kama ifuatavyo: Kumi ina tarakimu mbili (moja na sifuri
moja). Mia moja ina tarakimu tatu (moja na sifuri mbili). Elfu moja ina tarakimu nne (moja na sifuri tatu).
Elfu kumi ina tarakimu tano (moja na sifuri nne). Laki moja ina tarakimu sita (moja na sifuri tano). Milioni moja ina tarakimu saba (moja na sifuri sita).
Bilioni moja ina tarakimu kumi (moja na sifuri tisa). Trilioni moja ina
tarakimu kumi na tatu ( moja na sifuri kumi na mbili).
Kama
ulivyokwishaona, namba ya kiwango cha trilioni ni kubwa. Kuandika tarakimu kumi
na tatu bila kusahau au kuchanganya tarakimu si jambo rahisi. Wengine
hutenganisha namba hizo kwa alama ya mkato lakini utaratibu huo ulishapendekezwa
na shirika la kimataifa la viwango (ISO) uachwe. Mapendekezo hayo yametekelezwa
kwa mtaala wa Hisabati tu. Nyanja nyingine bado watumiaji hawajaanza kuutekeleza
na pengine hawautaki.Mfano ni wahasibu na benki. Hawa hata usipoiweka wataiweka
kulinda fani yao.
Kwa kutambua
tatizo hilo, namba kubwa hufanyiwa makadirio. Kwa mfano, tunaposema bajeti ya serikali ni shllingi za Tanzania trilioni
kumi na nane hatuna maana kwamba hakuna mamilioni au mabilioni. Zinaweza kuwepo
lakini kwa kuwa ziko chini ya nusu trilioni zikaachwa kutajwa kwa kukadiria trilioni
ya karibu. Au pengine ilikuwa trilioni kumi na saba na bilioni mia tano au
zaidi ya bilioni mia tano kwa hiyo ikakadiriwa kwa trilioni ya karibu kuwa trilioni
kumi na nane.
Unaweza pia
kutumia namba mchanganyiko kutaja namba kubwa kwa kukadiria. Kwa mfano, unaweza
kusema shilingi trilioni kumi bilioni mia tano ni shilingi trilioni kumi na
nusu. Pia namba hiyo inaweza kutajwa kwa desimali kwa kusema trilioni kumi nuka tano. Wabunge wengi
waliochangia mawazo yao katika bajeti hiyo wametumia mtindo huo. Huu ni mtindo
rahisi katika usomaji wa namba zenye tarakimu nyingi. Kwa mfano, namba
1367300000000 inaweza kusomwa: “trilioni moja nukta tatu sita saba tatu.”
Ningependa
kutahadharisha kuhus jambo jingine linalotatanisha wakati wa kusoma namba. Kuna
namba ambazo zikisomwa huweza kuandikwa tofauti na ilivyokusudiwa. Kwa mfano,
“elfu kumi na moja”. Mtu anayesikiliza anaandika 10001. Kumbe aliyekuwa anasoma
tarakimu ilikuwa imeandikwa 11000. Ndio sababu inashauriwa kwamba namba hiyo isomwe:
“kumi na moja elfu”.Hili tumeshaliona hapo juu.
Katika
muhtasari wa sekondari wanafunzi wanajifunza mada iitwayo kuandika namba kwa
mtindo wa kisayansi (scientific notation or standard form). Hii huwajengea
wanafunzi uwezo wa kuandika namba kubwa au ndogo sana kwa kuweka nukta baada ya
tarakimu na kuandika kwa kipeo kupata kiwango cha namba. Hii hurahisisha sana
kujuakiwango cha namba husika na husomwa kwa desimali. Kwa mfano,
18234000000000 huandikwa 1.8234x1013
na husomwa moja nukta nane mbili tatu nne mara kumi kipeo cha kuminna
tatu. Tunajua sasa namba lkiwa kwenye
kumi kipeo cha 13 ni kiwango cha trilioni
kumi.
Mwjsho ningependa
kushukuru kwa lugha yetu ya Kisahili kuwa na neno laki maalumu
kwa elfu mia. Sina uhakika kama Waingereza wanalo neno kama hilo. Tunaomba
BAKITA na wataalamu wengine waendelee kutafuta istilahi kwa ajili ya
kurahisisha uwasilishaji wa taarifa mbalimbali. Hili linawezekana. Tuongeze
bidii.
No comments:
Post a Comment