Sunday, 7 July 2013

CHAHITA NI CHAMA MUHIMU


CHAHITA ni kifupi cha Chama cha Hisabati Tanzania.  Kiliundwa Januari 1966 huko Chuo Kikuu cha Dar es Salaam wakati Walimu wa Hisabati kote nchini walipokutana kujadili masuala ya Hisabati mpya.  Mwaka huu chama hicho kinafanya kikao chake cha 47 huko Arusha katika Chuo Kikuu cha Makumira kuanzia tarehe 17/9/2012 hadi tarehe 22/9/2012. Mkutano huo unatarajiwa  kufunguliwa na Naibu Waziri wa Elimu TAMISEMI, Mheshimiwa Kassim Majaliwa (Mb).

 Japokuwa chama hiki kilianzishwa na wanahisabati, kwa sasa kimepanua uwigo wake na kinamfaa mtu yeyote mwenye mapenzi na somo la Hisabati.  Msukumo wa sasa ni kuendeleza juhudi za kuinua kiwango cha uelewa na utumizi wa Hisabati katika maisha. Pia chama hicho kimepania kuondoa fikra potofu kwamba chama hicho ni kwa walimu wa sekondari na wahadhiri wa vyuo vikuu tu. Jitihada zinafanyika ili walimu wa shule za msingi kushiriki maana somo hilo linaanzia shule za msingi.

MT/CHAHITA kimedumu kwa muda wote huo kutokana na wanachama wake kuwa waadilifu na uwezo wao wa kujitolea kwa hali na mali.  Kwa mfano, viongozi wa kitaifa wanaounda kamati kuu hukutana kila Jumatatu ya kwanza ya mwezi isipokuwa mwezi Oktoba.  Hawakutani Oktoba kwa sababu ndio tu wanakuwa wamerudi kwenye mkutano wa mwaka ambao hufanyika katikati ya mwezi Septemba.


Kumekuwa na uelewa tofauti kuhusu chama hiki.  Wako wanaodhania kwamba chama hiki ni kwa ajili ya walimu na wanafunzi wa sekndari na vyuo tu.  Ukweli ni kwamba chama hiki ni cha ngazi zote za elimu.  Japokuwa wengi wanaohudhuria mkutano wa mwaka hutoka katika shule za sekondari na hasa shule za bianfsi, mwaliko huenezwa kwa watu wote wakiwepo walimu wa shule za msingi.  Hata hivyo juhudi za kuwahusisha walimu wa shule za msingi bado hazijazaa matunda.

 Katika Kamati ya Taifa wako wawakilishi wawili wa shule za msingi, mmoja akitoka Dar es Salaam na mwingine mkoa wa Pwani.  Viongozi wa kitaifa hawatoki nje ya Dar es Salaam kutokana na kutokuwepo fedha za kulipia nauli ya wajumbe.  Shughuli zote zinafanyika kwa njia ya kujitolea. Mpaka sasachama hakijapata mdhamini lakini kinaendelea kutafuta.

Wako watu wanaoshangaa kwamba chama kimekuwepo kwa miaka yote lakini hali ya somo la hisabati inaendelea kuwa mbaya.  Baadhi yao wamekilaumu chama hasa waliposikia kwamba somo la Hisabati mwaka jana liliongoza kwa kufanya vibaya katika mtihani wa kumaliza elimu ya msingi ambako 17% tu walifaulu somo hilo.  Ukweli ni kwamba CHAHITA kimekuwa kikijaribu kwa kila njia kupambana na tatizo hilo bila mafanikio makubwa.  Kimekuwa kikiendesha semina kwa walimu, kuendesha shindano la hisabati kwa wanafunzi na kuchapisha majarida na vitabu kwa mada zimeonekana tata.

Kuazia mwaka2007 chama hicho kilianza kuendesa siku ya pai iliyoanzishwa hapa Tanzania na mratibu wa Hisabati Taasisi ya Elimu Tanzania mwaka2004. Siku ya pai imekuwa mojawapoya majukwaa ya chama hicho kuwakutanisha wadau wa Hisabati kufanya shughli mbalmbali za kuhamasisha wanafunzi kupenda somola Hisabati.

Tatizo ni kwamba huduma hii inawafikia watu wachache tu.  Kwa mfano, kwa ngazi ya msingi ambako ndio chimbuko la matatizo, ni wanafunzi au walimu wachache tu wameshafikiwa.  Baadhi ya kanda za CHAHITA zimeunda kanda ndogo katika ngazi ya wilaya ili kufanikisha azma hiyo kutokana na tatizo la umbali.  Ziko shule chache ambazo zimeunda klabu ili ziwahudumie wanafunzi vizuri zaidi.  Kwa jumla hali ni ngumu na chama peke yake hakiwezi kufanikisha bila kupewa uwezo wa ziada pamoja na ushirikiano.

Kutofanya vizuri katika mitihani kunasababishwa na mambo mengi yakiwepo  wanafunzi, kutolipenda somo, kutofanya mazoezi, ukosefu wa walimu na uhaba wa vitabu. Pia baadhi ya waalimu huwakatisha tamaa wanafunzi wenye uwezo mdogo katika somo hilo.  Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi (MEMU) imekwishaliona tatizo hilo na inalifanyia utafiti ili hatua muafaka ziweze kuchukuliwa kulinusuru somo na balaa iliyolikumba.  Ni dhahiri kwamba juhudi hiyo itahitaji kuungwa mkono na watu wote. Taasis ya Elimu Tanzaia (TET) imekuwa ikitoa semina kwa baadhi ya masomo,  likiwepo la Hisabati, ambapo huwalipia wataalamu (wawezeshaji) na washiriki kujilipia nauli na  kujikimu. Hata hivyo ni walimu wachache tu walioweza kujiunga na utaratibu huu. Wale walioweza kufanya hivyo walionyesha kuridhika na huduma hiyo. Katika mhadhara ambao CHAHITA huuita Mhadhara wa  mwaka, Profesa Ralph Masenge wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (Open University Of Tanzania) alishauri wadau wa elimu kujizatiti kukabiliana na tatizo hilo sugu. Alishauri MEMU kuwamotisha walimu ili wabakie kwenye ajira yao  badala ya kutafuta kazi nyingine zenye maslahi zaidi. Pia alishauri TET na Baraza la Mitihani wapewe uwezo wa kutunga mitaala na mitihani itakayoboresha somo la Hisabati ili wanafunzi wengi zaidi walipende. Walimu nao walihimizwa kubadili aina ya ufundishaji unaomfanya mwanafunzi kukariri na badala yake watumie njia shirikishi.
Mheshimiwa Kassim Majaliwa(wa pili toka kushoto) akimsikiliza mwanzishi wa Siku ya Pai Tanzania akiimba wimbo wa Pai katika uwanja wa Jangwani Shule ya Sekondari 2011.
 Katika semina ya mwaka huu washiriki waliweza kujifunza mada zinazowasumbua walimu  katika kuzifundisha. Katika ngazi ya shule za msingi walijifunza njia na mikakati mbalimbali za kufundisha na kujifunza jometri, aljebra na maumbo ya ukumbi. Walijifunza ‘spheres’ (tufe) na ‘accounts’ (hesabu za fedha) kwa sekondari kidato cha kwanza hadi cha nne. ‘Linear Programming,Probability and Vectors’ zilifunndishwa kwa ngazi ya kidato cha tano na sita. Pia washiriki walipata fursa ya kuona matumizi ya kompyuta katika uwasilishaji wa mada kwa kutumia ‘power point’. Walimu kadhaa walionesha zana za kufundishia mada tata. Profesa Ralph wa Chuo Kikuu cha Huria Tanzania aliyetajwa hapo juu, alitoa ‘mhadhara wa mwaka’ juu ya matokeo mabaya ya Hisabati katika mitihani ya taifa.

 Mkutano huo ulipambwa kwa nyimbo kutoka kwa wanafunzi wa shule ya msingi ya Mlimani ya huko Morogoro walioimba kusifia hisabati. Pia washiriki waliimba nyimbo za pai. Tunaamini wale wote waliohudhuria wataeneza ujumbe kwa wale ambao hawakupata fursa ya kuhudhuria. CHAHITA kiko tayari kusaidiana na wote wenye nia ya kuliokoa somo hilo katika dimbwi la matatizo.  Hisabati iko katika nyanja nyingi za maisha yako.  Usisite kutoa mchango wako pale unapoweza. Inawezekana. Anza leo. Wengine watakuunga mkono.

END


No comments:

Post a Comment