Saturday, 27 July 2013

Galileo Galilei: Wagunduzi 3

Beniel Seka
Sayansi ya kisasa ilianzishwa na watu waliouliza maswali a yaliyohitaji uchunguzi kuliko ya wale waliotangulia. Kulikuwa na mapinduzi ya fikra za sayansi karne ya kumi na sita na ile ya kumi na saba. Mwanasayansi maarufu alikuwa mmoja wa wale walichangia sana katika mabadiliko hayo.
Galileo Galilei alizaliwa mwaka 1564, mwaka aliofariki mtu marufu aitwaye  Michelangelo. Alikufa mwaka 1642, mwaka aliozaliwa mwanasayansi mkongwe, Isaac Newton. Baba yake alikuwa mtu maarufu wa Florence nchini Italia. Galileo alipata elimu bora,kwanza katika uganga katika Chuo Kikuu cha Pisa na baadaye alisoma Hisabati na Fizikia.
Ugunduzi wake wa kwanza ni ule wa ‘pendulum’. Ukitaka kujua zaidi, funga jiwe dogo wa kamba na unin’ginize kwenye sehemu ambapo linaweza kujongea pande zote. Sukuma jiwe kidogo ili licheze pande zote hadi litulie kutokana na ukinzani wa hewa. Kama kusingekuwa na hewa tukio hilo lingendelea bila kukoma.
Ugunduzi wake wa pili uliomfanya maarufu ni uvumbuzi wa msawazo majituli (hydrostatic balance). Pia aliunda saa ya pendulum na kipimajoto (thermometer) cha kwanza. Alitengeneza mrija wa kioo angavu ambacho upande mmoja ulifunikwa kwa kioo cha mviringo mithili ya balbu. Aliweka maji kama kimiminika cha kuhisi joto. Siku hizi tunatumia zekaki. Vilevile, kwa kutumia elimu ya kupinda kwa mwanga unapopita maada angavu tofauti, alitengeneza moja ya hadubini na darubini za kwanza. Hata hivyo utambuzi zaidi alipewa Mdachi Jan Lippershey kwa ugunduzi wa vifaa hivi. Huenda Galileo alichelewa kuutangaza.
Kuanzia mwaka 1592 hadi 1610, Galileo alikuwa Mwenyekiti wa Hisabati Chuo Kikuu cha Padua. Alikuwa mhadhiri aliyependwa sana. Ilibidi ukumbi wa kuchukua watu takriban 2000 utengwe kwa ajili ya wahudhuriaiji wa mihadhara yake.
Kionambali chake kilimfanya awe na wasiwasi na nadharia ya Ptolomy iliyodumu miaka mingi. Nadharia hiyo ilisema Dunia ni kitovu ambapo sayari, nyota , jua na mwezi huizunguka. Alianza kukubali nadharia iliyopendekezwa na Nicholas Corpenicus iliyodai kuwa jua liko katikati na huzungukwa na dunia na sayari. Mwaka 1604 alitangaza rasmi kukataa nadharia ya Ptolomy.
Aliikarabati darubini yake ya mwanzo na kufanya gunduzi zilizofungua ukurasa mpya katika historia ya astronomia. Aligundua miezi (setilaiti) 4 kati ya 11 ya sayari ya Sumbula (Jupiter); madoa ya jua na mabadiliko ya mwonekano wa sayari ya Venus kama yaonekanavyo yale ya mwezi wetu. Hiyo pia ilisaidia kudhihirisha wazo alivyokuwa ametabiri Corpenicus.
Mwaka 1615 aliondolewa Padua na kurejea Florence. Kuunga mkono mawazo ya Copernicus kulianza kumsababishia mgogoro na kanisa lake. Alipewa onyo lakini aliruhusiwa kuandika kwa uhuru, ila alipewa masharti kuwa asihusishe masuala ya mambo matakatifu katika maandiko hayo. Alifanya safari mbili Rome kueleza msimamo wake kwa Papa Mtakatifu. Safari ya pili alikutana na Papa Mtakatifu Urban  VIII ambaye alimkaribisha vizuri.
Alipochapisha andiko lake liitwalo ‘Dialogue on the Great World Systems’ (Mazungumzo ya Mifumo ya Dunia Kubwa), mwaka 1632, aliwasha moto mkali wa kimahusiano kati yake na kanisa. Aliitwa Rome na kushtakiwa kwa kueneza uvumi. Alilazimishwa kukiri kosa na kupewa kifungo cha nyumbani cha maisha. Alirudi kwenye nyumba yake karibu na Florence kutumikia adhabu yake. Aliishi pale maisha ya upweke sana. Mwaka 1637 alikuwa kipofu na akafariki miaka mitano baadaye akiwa na miaka sabini na nane.


No comments:

Post a Comment